Pages

Wednesday, 18 December 2013

JAJI WEREMA NA ZITTO NANI ANASEMA UKWELI?



        Bila ya kuwataja kwa majina, Zitto alisema watu hao ni wale walioshika nyadhifa za uwaziri mkuu katika kipindi cha 2003 hadi 2010, walioshika nyadhifa za uwaziri wa nishati na madini katika kipindi hicho na waliokuwa makatibu wakuu Wizara ya Nishati na Madini.
Wengine ni mawaziri na makatibu wakuu wa Wizara ya Ulinzi, wakuu wa majeshi, wanasheria wa Serikali, makamishna wa nishati na walioshika wadhifa wa Ukurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC.
Baada ya kutolewa kwa hoja hiyo, Serikali iliunda kikosi kazi cha kufuatiliwa fedha hicho, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Fredrick Werema akiwa ndiyo kiongozi wa timu hiyo.
Katika mahojiano ambayo Jaji Werema alifanya na Mwananchi mapema Januari mwaka huu, alisema hadi kufikia Aprili mwaka huu, wangekuwa na jambo la kueleza umma kutokana na uchunguzi huo.
Werema abainisha kuwa Serikali iliandika barua kwa vyombo vya Uswisi vinavyohusika na masuala ya fedha, wakivitaka viwape taarifa za akaunti za Watanzania.

 
“Walitueleza tunachojaribu kufanya ni sawa na mtu anayevua samaki, anajua kabisa kuwa baharini kuna samaki, lakini mahali walipo hapajui. Walitaka tuwape majina ya wahusika tunaowataka, kisha kuwaeleza kwa nini tunazitaka fedha hizo,” anaeleza na kuongeza:
Anasema katika kufuatilia hilo, wangekwenda mbali zaidi kwa kufuatilia majina yote watakayopata na kuangalia wahusika kama wana kibali cha Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuweka fedha hizo katika nchi hiyo.
Anasema kuwa Zitto Kabwe ambaye ndiye aliyeeleza suala hilo bungeni ni mtu muhimu kwao, hivyo angeshirikishwa ipasavyo.
 “Tukipata taarifa kwa sasa tunaweza kwenda kwenye hizo benki, hatutaki kwenda tu na kusema tupewe majina ya Watanzania walioweka fedha zao huko, ukifanya hivyo kama huyo mtu atakuhurumia sana sana atakufukuza, lakini kama ni mweledi atakuitia polisi,” anasema Werema.
Kauli hiyo ya Werema, ilikuja siku chache baada ya Balozi wa Uswisi nchini, Olivier Chave kusema Serikali ya Tanzania haijaonyesha nia ya dhati kutaka kuchunguza na kupata ukweli wa mabilioni ya fedha yaliyofichwa nchini humo.
Chave anasema: “Uswisi iko tayari kushirikiana na Tanzania kujua uhalali wa fedha hizo na endapo zikigundulika ni fedha chafu basi tutazirejesha nchini.

Serikali ya Uswisi haina tatizo kwani tumeshafanya hivyo kwa nchi za Ufilipino na Nigeria, hivyo tutafurahi na Tanzania kama tutamaliza suala hili,” alisema balozi huyo.
Mbali na balozi huyo, Rais wa Bunge la Uswisi, Maya Graf mwisho wa Oktoba alifanya mazungumzo na gazeti hili ambapo pia alizungumzia suala hilo.
Alipoulizwa kama anafahamu kuwa, kuna hoja binafsi ndani ya Bunge la Tanzania juu ya fedha zilizofichwa nchini mwake, alisema kuwa hilo siyo suala la Bunge, bali ni suala kati ya Serikali ya Uswisi na ile ya Tanzania.
“Serikali yetu ni ya uwajibikaji. Nina uhakika kama Serikali itakuwa imeelezwa itafanya kazi yake,” anasema.
Kauli ya Werema aliyoitoa Januari iliwapa Watanzania matumaini, lakini mpaka Bunge la Aprili linapita hakuna kilichofanywa.
 
Baada ya hapo, Zitto alinukuliwa mara kadhaa akiahidi kuwa siku moja atayataja majina ya watu walioficha fedha hizo, huku akiilaumu Serikali kutokufanya kazi yake kama ilivyotarajiwa katika kufuatia fedha hizo.

Zitto asisitiza

Juma lililopita akizungumza bungeni, Zitto anaihoji Serikali akiktaka ieleza sababu za kuchelewesha ripoti ya ufichaji  wa fedha nje ya nchi.
Anasema tatizo ni utayari wa Serikali katika kulishughulikia jambo hilo na kuhakikisha linaisha.
Anasema kuna mikataba kwa ajili ya kupeana taarifa na Afrika zimesaini ambazo ni Ghana, Afrika Kusini na Nigeria, lakini Tanzania haijaisaini.
“Utapataje taarifa wakati hujasaini mkataba kama huu, mjadala sasa ni mabilioni ya fedha za Uswisi lakini ni zaidi ya mabilioni ya Uswisi. Uswisi kuna Sh319 bilioni, Genes, kisiwa kimoja nchini Uingereza kina zaidi ya trilioni moja za Watanzania na ukikaa mtajadili na Watanzania na wanapenda vitu vyepesi vyepesi.”

Majibu ya Werema 

 

Jaji Werema akijibu hoja za Zitto mbali na kuomba kuongezewa miezi sita ili wamalize suala hilo, anapinga suala la Tanzania kusaini sheria ya kubadilishana taarifa za fedha.
 “Leo anataka (Zitto) tuangalie mfumo badala ya majina, nakumbuka katika Bunge la Tisa, mimi nilikuwa nasema tuangalie mfumo lakini Zitto akasema umefika wakati wa yeye kutoa dukuduku lake atoe taarifa zake na nyaraka alizonazo ili watu hao washughulikiwe.”
Werema anasema kuwa, katika kujaribu kupata taarifa kwa Zitto, mbunge huyo amekuwa akiwakwepa tangu Februari na kuwa, mwishowe mbunge huyo alikiri kwa kiapo mbele ya kamati hiyo kuwa hana majina wala akauti za fedha hizo.
Ikumbukwe, awali, Werema alisema, Zitto angekuwa tu sehemu ya watu wanaosaidia timu hiyo, lakini kauli yake bungeni juma lililopita, inaonekana kama Zitto ndiye aliyekwamisha zoezi zima la utafutaji wa fedha hizo.
Werema hakuzungumza hata kidogo juu ya nini ambacho mpaka sasa tume yake aliyosema imejaa watalaamu wamefanya, zaidi alitaka aongezewe miezi sita ili akamilishe kazi hiyo.
Inabidi Werema aseme ni nini kinamkwamisha kumaliza kazi hiyo ilihali ana kila kitu kinachotakiwa, fedha pamoja na watu wa kuifanya shughuli hiyo. Pia kwa nini serikali inasita kusaini sheria hiyo ya kubadilishana taarifa za kifedha kweli itakuwa njia rahisi za kupata taarifa hiyo.
Kwani licha ya kuwa na rasilimali zote, anang’ang’ania Zitto ataje majina, kama njia pekee ingekuwa ni mbunge huyo kutaja majina hayo, kwa nini kamati hiyo iliundwa?
Maswali haya yanafanya watu waamini kuwa, watu walioficha fedha hizo nje ya nchi yawezekana wanab mkono wao katika kukwamisha suala hili.

0 comments:

Post a Comment