Pages

Friday, 17 January 2014

UCHAMBUZI WA MAKALA


                    GOLOSO LA SPORT
                                                  
              NA (YUDATHADEI KWAY)
       

    JE NI KWELI MOYES NI MRITHI WA FERGUSON?

Inaaminika na walio wengi ya kwamba mtu makini anaelezea maendeleo katika wakati uliopo kwenye nyanja yoyote ile ni vyema akawa anatoa na historia ya hali ilivyokuwa katika kipindi cha nyuma. Kwa kuanza hivyo sinabudi ninapotaka kumgusia David Moyes kumzungumzia Sir Alex Ferguosn pindi akiwa kama meneja wa Manchester United.
Jina halisi la kocha huyu mstaafu na aliegusa kiaina yake mioyo ya wadau wa soka ni Sir Alexander Chapman ‘’Alex’’ Ferguson. Alijiunga na kikosi cha Man U mnamo November 1986 kama mrithi wa kocha Sir Matt Busby. Kipindi akipewa timu hii hali ilikuwa mbaya kisoka klabuni hapo mbali na changamoto hiyo alikuta wachezaji hawana nidhamu ya kutosha kama vile kuwa na wachezaji walio walevi wa kupindukia akina Norman Whiteside, Paul McGrath na Brayan Robson hali hii ilimtisha sana kocha huyu ila alijitahidi vilivyo katika kukabiliana na hali ya nidhamu.
Kipindi akikabidhiwa mikoba timu ilikua katika nafasi ya 21 ya pili kutoka mwisho, Kocha huyu alijitahidi na akiwa na wachezaji hawahawa hadi kujikita katika nafasi ya 11 katika msimu wa 1986/1987 hali iliokuwa ya kutia moyo kwa waajiri wa kocha huyu na hata kwa mashabiki wa timu hii. Katika msimu uliofuata wa 1987/1988 kocha huyu aliongeza nguvu kwenye kikosi kwa kuwasainisha mkataba wachezaji wanne Steve Bruce, Viv Anderson, Brian McClair na Jim Leighton. Nguvu hii iliiwezesha timu hii kufikia nafasi ya pili ya msimamo wa ligi points 9 nyuma ya Liverpool. Msimu uliofata 1988/1989 kocha huyu alimrejesha klabuni hapo Mark Hughes kutokea Barcelona lakini hali haikuwa nzuri sana kwa klabu hii kwani ilimaliza msimu wa ligi kuu kwa kuwa katika nafasi ya 11.
Katika msimu wa 1989/1990 kocha huyu alifanya kufuru kwa kuvunja sefu ya klabu hii kwa kuwasajili Neil Webb, Mike Phelan, Paul Ince na winga machachari Danny Wallee. Hali haikuwa kama matarajio yake na wafuasi wake yalivyolenga kwani katika mechi nane za kwanza za ligi kuu timu ilifungwa mechi 6 na kudroo mbili. Mashabiki na vyombo vya habari kwa pamoja vilimshambulia vikali na hata wengi wao kudai board ya klabu hio imuondoshe katika wadhifa wake kama kocha, Lakini board haikuwa na papara kwani walimuahakikishia kocha huyu msikochi kutofukuzwa kwani waliikubali sababu yake yakuwa timu ilifungwa kutokana na kwamba wachezaji muhimu walikuwa wakisumbuliwa na majeraha. Hali hii ilimpatia amani na kujiamini katika kazi yake na mwisho wa siku alifanikiwa kuchukua kombe la ‘’FA Cup’’ kwa kuifunga timu ya Crystal Palace bao 1-0 katika mechi ya marudiano baada ya kutoka 3-3 katika mechi ya kwanza. Katika msimu uliofuata wa 1991/1992 klabu ilifanikiwa kubeba vikombe viwili UEFA supercup na League Cup. Katika msimu wa 1992/1993 Kocha huyu alimsainisha straika makini kabisa mfaransa akitokea Leeds United kwa kitita cha Euro million 1.2, huyu ndiye Eric Cantona. Mpachika mabao huyu aliweza kuuwasha moto katika safu ya ushambuliaji akiwa na mchochea kuni wake Mark Hughes na mwisho wa msimu klabu hii iliweza kufanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Uingereza na kukata kiu cha muda mrefu kabisa, takribani miaka 26 bila kutwaa kombe hilo.
Katika msimu uliofuata klabu hii ilimsajili Roy Kean kwa kitita cha Euro Million 3.75, katika msimu huu klabu iliweza kuchukua vikombe viwili. FA cup kwa kuichapa Chelsea 4-0 katika fainali na Kutwaa kwa mara nyingine kombe la ligi kuu na kumtoa mfungaji bora Erick Cantona.
Mafanikio yaliendelea kudhihirika chini ya kocha huyu na kutia fora katika msimu wa 1998/1999 kwa kuchukua vikombe vitatu kwa mkupuo, kuanzia klabu bingwa Ulaya(UEFA) ligi kuu Uingereza na FA Cup.
Tayari kocha huyu aliweza kukonga nyoyo za wadau wa soka, sio wale tu waliokuwa  kama mashabiki wa Man U lakini hata mashabiki wa klabu nyingine na hata kudhihirisha ubora na ukomavu wake katika soka. Lilikuwa pigo ambalo si rahisi sana kufutika kwa miaka ya hivi karibuni katika tasnia ya soka la vilabu, soka linaloaminika kuwa msingi bora kwa kukua kwa soka katika michuano ya mataifa mbalimbali kama kombe la dunia na hata makombe ya mabara kwa kocha huyu kuamua kustaafu na kumpendekeza aliyekuwa kocha wa Everton kwa kipindi hicho David Moyes kuwa mrithi wa mikoba yake.
Baada ya kuitizama historia fupi ya Kocha babu Sir Alex akiwa na kikosi cha Man U tujaribu kumgeukia kocha mrithi aliepewa jina la ‘’Dithering Dave’’ na mashabiki wa Everton. Kocha huyu aliweza kufanya makubwa akiwa na kikosi cha Everton alicho kabidhiwa mwaka 2002 na hata kufanikiwa kuipeleka timu hio katika michuano ya klabu bingwa katika mwaka 2005 na hata kufikia hatua ya fainali katika kombe la FA mwaka 2009. Kocha huyu alidhihirika kuwa kati ya makocha bora kwa vigezo kwa kuwa hakuwa na wachezaji wa gharama sana katika kikosi chake na bado waliweza kutandaza soka maridadi kabisa katika ligi kuu ya Uingereza. Timu yake iliweza kuwa ndani ya kumi bora katika misimu mingi tu ya ligi kuu.
Kocha huyu tokea amekabidhiwa kikosi cha Man U hajaweza kudhihirisha ubora wake kwani ameishia kupoteza mechi nyingi katika michuano mbalimbali, ikiwemo kutolewa katika kombe la FA na kufungwa mechi ya nusu fainali ya mkondo wa kwanza  kombe la Capital One. Bado kocha huyu analegalega katika EPL akitoa matamko ya kuwa timu ni dhaifu. Maswali yanaibuka, ni vipi anasema timu ni dhaifu alihali Kocha aliepita alitumia wachezaji hawa hawa kutwaa ubingwa wa EPL? Kama aliona timu ni dhaifu ni kwanini hakufanya usajili katika majira ya joto? Je ataweza kusajili watu makini katika dirisha hili dogo? hapa ndipo zinakuja zile sababu za ukomavu na ubora wa kocha aliyepita. Mengi yanaongelewa na mengi yanatokea ikiwemo kushuka kwa mapato ya klabu na hata mashabiki kukosa morali ya kuishabikia timu yao kwa kifua mbele kama ilivyokuwa enzi za Kocha Sir Alex. Man U ni kati ya klabu zinazo sifika kwa uvumilivu kwa makocha wake, bado ni mapema kwa kocha huyu kufungashiwa virago tukirejea katika historia ya klabu lakini pia kwa kocha mwenye hekima kisoka ni muhimu kutumia mbinu mahususi katika kurejesha ubora na umakini wa klabu kama ilivyokua imetengenezwa na kocha mstaafu Sir Alex Ferguson.

   MWANDISHI WA MAKALA HII NI MSANIFU WA GOLOSO KWA HABARI ZA KIMATAIFA
                                                 0768-154424
 

0 comments:

Post a Comment